Monday, October 15, 2012

Wataka madaraka ya rais yapunguzwe





WAKAZI wa Wilaya ya Nachingwea, mkoani Lindi, wametaka katiba mpya ijayo, madaraka ya rais wa nchi ya kuteua watendaji wakuu yaangaliwe upya na ikiwezekana yapunguzwe.
Wakitoa maoni yao juzi katika mdahalo wa katiba mpya ulioendeshwa na Mtandao wa asasi za kiraia Mkoa wa Lindi (Lango), wakazi hao walilishukuru shirika hilo kuwapa nafasi hiyo ya kutoa maoni kutokana na kuikosa wakati tume ya kukusanya maoni ilipopita mkoani humo hivi karibuni.
Mmoja wa wakazi hao, Mawazo Hashimu mkazi wa Nachingea, alisema kuwa katika katiba ijayo, iko haja ya rais kupunguziwa madaraka ya kuwateua watendaji na kuwepo na ukomo wa madaraka.
“Rais asiwateue wabunge kuwa mawaziri, kwani hao ni watetezi wa wananchi na wawakilishi wao bungeni… sasa rais atakapowateua kuwa mawaziri hawatapata muda wa kuwatetea wale waliowachagua,” alisema.
Aidha, wananchi hao walipendekeza kuwepo na ukomo wa madaraka ya viongozi kwani wamekuwa wakiongoza nchi kwa miaka 30 hadi 40.
Wananchi hao waliongeza kuwa katiba hiyo iwabane wabunge kuishi majimboni kwao kama ilivyo kwa madiwani badala ya sasa ambapo wengi wao wamekimbia majimboni na kuhamia jijini Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment