Saturday, October 20, 2012

DK. HELEN BISIMBA: Mwanaharakati mtetezi wa haki za binadamu




HELEN Kijo Bisimba, ni jina linalosikika ndani na nje ya Tanzania. Huyu ni mama shupavu, jasiri, mpambanaji na mwanaharakati wa kutetea haki za binadamu, ambaye ameamua kujitoa kutoa mchango wake katika kuendeleza na kulinda ustawi wa taifa la Tanzania.
Tumezoea kusema kwamba ‘nabii hasifiki nyumbani’! Inawezekana ni hivyo kwa mama huyu, ambaye kazi anazozifanya zinaheshimika na kusifiwa kwenye ulingo wa kimataifa kuliko hapa nyumbani? Inawezekana ni kwa vile kazi anayoifanya mama huyu inaigusa serikali jichoni au kwa vile amejifunga kibwebwe kupambana na mfumo dume na kutaka kuutokomeza? Au labda ni kwa vile bado viongozi wengi kwenye ngazi ya maamuzi katika taifa letu ni wanaume?
Juzi, sote tumeshuhudia kwenye vyombo vya habari Dk. Bisimba akisoma taarifa ya Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kuamua kuiburuza Serikali ya Tanzania kwenye Mahakama ya Uhalifu ya Kimataifa (ICC) iliyoko The Hague, Uholanzi.
Hiki ni kitendo cha ujasiri na kujitoa, maana ni wachache wanaoweza kuthubutu kufanya hivyo bila kuogopa matokeo yake.
Hata hivyo, Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu, kinachoongozwa na Bisimba, kimekuwa mstari wa mbele kutetea haki za watoto, wanawake na watu wote wanaokandamizwa; kunyang’anywa ardhi yao na matuko mengine ya kifisadi yanayoendelea katika taifa letu. Kituo hiki kimekuwa sauti ya wanyonge.
Mama huyu amejitofautisha na baadhi ya watu wanaoongoza mashirika yasiyo ya kiserikali (NGO’s) mbalimbali katika taifa letu la Tanzania; hata kama NGO’s hizo zinakuwa ni za kutetea haki za binadamu, viongozi hao wamekuwa wakifanya kazi kwa malengo ya kupata mshahara tu!
Au kwa lengo la kujenga majina yao na kujitafutia sifa. Ni tofauti kabisa na Bisimba, ambaye Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kimekuwa sehemu ya maisha yake.
Bila unafiki na kujipendekeza, Bisimba anaonekana wazi kuguswa na kila aina yoyote ile ya ukiukwaji haki za binadamu katika taifa letu. Amekuwa mstari wa mbele kupinga ufisadi, rushwa na uporwaji wa rasilimali katika taifa letu.
Ameshiriki kuipigania demokrasia na utawala bora na kilio cha katiba mpya katika taifa letu. Haogopi kusimama na kusema wazi msimamo wake na msimamo wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu.
Yuko tayari kusema hata yale yasiyopendeza kwenye masikio ya watawala.
Mama huyu aliyezaliwa mnamo mwaka wa 1954 mkoani wa Kilimanjaro, ndiye Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kinacholinda na kutetea haki za binadamu za kila Mtanzania na kuhakikisha kwamba kila raia anakingwa na aina zote za udhalilishaji.
Mapenzi ya kutetea haki za binadamu na moyo wa unaharakati yalionekana kwake kwenye miaka ya 1970 alipokuwa akisoma sekodari ya Korogwe kule Tanga.
Alifukuzwa shule kwa muda, baada ya kukataa shinikizo la walimu wake kuomba msamaha kwa barua ya kudhalilisha aliyoandikiwa mwalimu mkuu wa shule. Alikataa kuomba msamaha wa kosa ambalo yeye hakutenda.
Kwa vile alikuwa msaidizi wa kiranja wa shule alikubali kufukuzwa kuliko kuomba msamaha. Baba yake mzazi alikwenda kumwombea msamaha, lakini walimu walikataa. Hadi alipoamua baadaye kuzungumza na walimu na hatimaye kuomba msamaha kwa kosa ambalo hakulitenda mwenyewe.
Tukio hili lilimjengea moyo wa ujasiri ambao hadi leo hii zaidi ya miaka 40, amekuwa akitetea haki za wanyonge, wanaume kwa wanawake, vijana kwa wazee.
Mama huyu, alikuwa kati ya watu wa kwanza kumshughulikia Dk. Stephen Ulimboka alipotekwa, kupigwa na kuteswa.
Kila mtu alishangaa jinsi mama huyu alivyopata habari haraka juu ya tukio hilo la kinyama na kufanya haraka kushiriki kutoa msaada kwa Dk. Ulimboka.
Alimsaidia kumfikisha hospitali na kuendelea kuishinikiza serikali ifanye uchunguzi wa kina kubaini watu waliofanya unyama huo.
Wakati wa mgomo wa madaktari, sauti ya Bisimba ilisikika kote kwenye vyombo vya habari. Yeye na wanaharakati wengine waliishinikiza serikali kufanya haraka kuumaliza ili kunusuru uhai wa raia wasiokuwa na hatia.
Na katika hali isiyokuwa ya kawaida mama huyu na wanaharakati wengine walikamatwa na polisi na kuhojiwa wakati walipofika Muhimbili, kutaka kujua kinachoendelea.
Mwaka 2001, alikuwa mwanamke mwanaharakati wa kwanza kupinga na kulaani mauaji yaliyotokea Zanzibar. Kitendo hicho kilimletea sifa ndani na nje ya Tanzania.
Mwaka 2008 alikuwa mwanamke wa kwanza kupokea tuzo ya Mwanamke Jasiri inayotolewa na Balozi wa Amerika nchini Tanzania.
Mama huyu amekuwa mstari wa mbele kupinga hukumu ya kifo. Siku ya Kupinga Hukumu ya Kifo inaangukia siku yake ya kuzaliwa ambayo ni Oktoba 10, hivyo mwaka huu anapoadhimisha miaka 58 ya kuzaliwa, ana imani kubwa kwamba iko siku adhabu hii ya kifo itakuja kufutwa nchini Tanzania.
Mama huyu ni kati ya watu wanaotamani kuona Tanzania inawaruhusu wasichana wanaopata mimba wakiwa shuleni kuendelea na masomo, na elimu ya kujitambua inafundishwa shuleni.
Kwa maoni yake, wakati mwingine wasichana wanapachikwa mimba kwa kuwa na uelewa mdogo juu ya kujamiana; na kwamba wazazi wasione aibu kuongea na watoto wao juu ya suala la kujitambua na mahusiano, maana ukimya katika hili ni hatari zaidi kuliko faida.
Mama huyu yuko mstari wa mbele kupinga vifo vya wanawake wakati wa kujifungua na vifo vya watoto wadogo. Ameunga mkono na kushiriki kampeni zote zinazoendelea za kupambana kupunguza vifo vya wajawazito.
Pia kwa kupitia Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu anaongoza kampeni ya kutokomeza ukeketaji, kuwarithi wajane na aina nyingine ya unyanyasaji kwa wanawake.
Mama huyu alianza kukiongoza Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu mwaka 1996, na ni mmoja wa waanzilishi wa kituo hiki cha kutetea na kulinda haki za binadamu.
Ni mjane tangu mwaka 1994. Ana watoto wanne, wawili ni mainjinia, mmoja ni daktari na mwingine ni mhasibu. Lakini pia anatunza watoto yatima nyumbani kwake na ni mwanachama wa wanawake wajane katika kanisa anapoabudu.
Mbali na kuwatunza watoto yatima nyumbani kwake, yeye amekuwa sauti ya watoto wanaojilea na kujitunza.
Wakati kuna watafiti wanaopinga Tanzania kuwa na familia za watoto wanaojilea wenyewe na kujitunza, Bisimba anaamini kwamba Makete na Karagwe, alikofanyia utafiti wa tasinifu yake ya shahada ya uzamifu, kuna familia za watoto wanaojilea na kujitunza kutokana na janga la ugonjwa wa ukimwi.
Mwaka 2008 mpaka 2001, alichukua likizo ya masomo na kwenda Uingereza kuchukua shahada ya uzamifu kwenye sheria na haki za binadamu.
Tasinifu yake ulikuwa ni utafiti juu ya haki za watoto. Alitaka sauti ya watoto wa Afrika isikike, alitaka kujua jinsi watoto wanavyouelewa mfumo wa serikali. Anaamini kwamba kwa kuelewa mawazo ya watoto, serikali yoyote inaweza kutenda vizuri siku zinazokuja, maana watoto wa leo ndio viongozi wa kesho.
Kabla ya kujiunga na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu, mama huyu alikuwa mwalimu wa Kiingereza na Kiswahili katika Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima alikofanya kazi kwa kipindi cha miaka 10.
Marehemu mume wake ndiye aliyemshauri kusomea sheria. Wakati anajiunga na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu, alikuwa bado anafundisha taasisi na kujitolea kwenye Shirika la WILDAF (Women in Law and Development in Africa) ambalo aliliwakilisha kwenye mkutano wa wanawake wa Beijing mwaka 1995.
Mama huyu ni kiongozi wa mfano. Hata wafanyakazi wenzake wanampenda na kumheshimu. Wengi amewaambukiza roho ya kutetea haki za binadamu na ujasiri wa kusimama kidete mbele ya haki.
Ukifika Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu, unakutana na mkurugenzi ambaye licha ya kuwa kiongozi wa kituo hicho, ni mama mwenye sifa zote za umama; kulea, kuelekeza, kujali, kutokuwa na uroho wa elimu, kuwashughulikia wengine, kuguswa na matatizo ya wengine na kuambukiza roho ya ujasiri kwa wafanyakazi wenzake.
Mama huyu pamoja na kazi kubwa alizonazo za kukiongoza kituo, bado ana nafasi ya kuihudumia familia yake, kuangalia mpira na watoto na wajukuu zake na pia kupata nafasi ya kuimba kwenye kwaya ya kanisa.
Huyo ndiye Bisimba, mwanamke shujaa, jasiri, msomi, mzalendo, mwanaharakati na mtetezi wa haki za binadamu.

No comments:

Post a Comment