|
VYOMBO vingi vya habari juzi vimetawaliwa na habari inayomhusu
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari, Dk. Stephen Ulimboka, ambaye ameweka
bayana kile kilichomsibu usiku wa Juni 26 mwaka huu, katika msitu wa
Pande nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.
Dk. Ulimboka ameeleza mambo mengi ikiwa ni pamoja na kuwataja kwa
majina baadhi ya watendaji wa Ikulu ambao anaamini kuwa walihusika kwa
namna moja ama nyingine katika tukio la kutekwa, kuteswa na kuumizwa
kwake.
Tunampongeza Dk. Ulimboka kwa kuweka bayana kile anachokiamini kuwa
ndiyo ukweli wa tukio la kutekwa kwake, kwani tunadhani sasa atakuwa
amefungua milango ya sakata hilo kuchunguzwa kwa umakini kukata mzizi wa
fitina.
Ni kweli kesi ya tukio hilo imefunguliwa mahakamani ambapo raia mmoja
wa Kenya anashtakiwa kufanya tukio hilo, lakini bado haizuii uchunguzi
wa kina kuendelea hasa wakati huu ambapo muhusika amejitokeza wazi kutoa
ushirikiano wa kuwatambua wale waliomfanyia kitendo hicho.
Tume ya uchunguzi iliyoundwa na Jeshi la Polisi kuchunguza tukio hio,
imekuwa ikinyooshewa kidole na baadhi ya wadau wakiwemo madaktari
wenyewe kwa madai kuwa haiko huru kwani baadhi ya wajumbe wake ni
watuhumiwa.
Hata Dk. Ulimboka katika taarifa yake hiyo ya jana, amesisitiza kuwa
yuko tayari kutoa ushirikiano wa kina endapo kitaundwa chombo huru
kuchunguza tukio hilo.
Ni vyema serikali ikajitafakari upya ili kuondoa sintofahamu hii
vinywani mwa watu kwa kuunda chombo huru ili kuchunguza sakata hilo na
hivyo kumfanya Dk. Ulimboka na Watanzania wengine kujiona wana haki ya
kuishi kwa amani katika nchi yao.
Dk. Ulimboka ameeleza wazi kuwa anathibitisha kwamba Ramadhani Ighondu
alitambulishwa kwao kwa jina la Abeid. Kwamba Binafsi anamfahamu sana
bwana huyu kwa sababu alikuwa akitumwa mara kwa mara kuja kukutana naye
na wamekutana mara kadhaa kabla ya tukio lile.
Alisema wazi kuwa anakumbuka kuwa Abeid alitambulishwa kwao na kigogo
mmoja, akiwa pamoja na wawakilishi wengine wa madaktari kuwa yeye
(Ramadhani Ighondu) ndiye atakayehusika katika kuchukua madai na hoja za
madaktari katika mgogoro kati ya madaktari na serikali.
Kwamba anathibitisha kwamba mfanyakazi huyu wa Ikulu, ndiye
aliyempigia simu na kumuita kwenye kikao ambako muda mfupi baadaye
alitekwa. Katika mawasiliano hayo, Abeid alikuwa anatumia simu namba
0713 760473.
Dk. Ulimboka amebainisha kwamba hakuna shaka kwamba anamtambua Abeid
kwa sura na namba aliyokuwa anatumia kuwasiliana naye mpaka siku ya
kutekwa kwake.
Hivyo, kwa maelezo hayo ya Dk. Ulimboka, hatuhitaji kuibua mijadala ya
malumbano ya nani kafanya nini na nani hakuhusika, isipokuwa jambo la
msingi hapa ni kuundwa chombo huru kitakachokuja na majibu ya kumaliza
utata huu, ndiyo maana tunasema Dk. Ulimboka amefungua milango ya
uchunguzi.
|
No comments:
Post a Comment