|
KADA wa Chama cha Mapinduzi (CCM), David Msuya, amemtaka Waziri
Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye, kuwataja waliotoa rushwa katika uchaguzi
wa viongozi wa CCM mwaka huu.
Msuya ametoa kauli hiyo ikiwa ni siku chache baada ya Sumaye kueleza
sababu zilizochangia ashindwe uchaguzi wa nafasi ya ujumbe wa
Halmashauri Kuu (NEC) ya CCM, wilaya ya Hanang, kuwa unatokana na
vitendo vya rushwa.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Msuya
ambaye pia ni mkurugenzi wa vikundi vya maendeleo ya wanawake (Inuka),
alisema badala ya kulalamika, Sumaye anatakiwa awataje wala rushwa na
watoa rushwa walioko ndani ya chama hicho, ili wachukue hatua kwa mujibu
wa sheria.
“Sisi Watanzania hatupendi rushwa maana ni adui wa haki, hivyo si
busara kuongea tu badala ya kuchukua hatua kwa kuwa yeye ni kiongozi
mkubwa mwenye sauti serikalini ambaye kama analalamika na sisi
tufanyeje? Kwa hiyo anatakiwa kupeleka suala hilo kwenye vikao vya
chama,” alisema.
Aidha, Msuya aliitaka serikali ikae na viongozi wote wa dini katika
kukemea vitendo vya vurugu vinavyoweza kujitokeza na kuharibu amani ya
nchi kutokana na vurugu za kidini zilizoibuka hivi karibuni ambapo
makanisa na vitu mbalimbali ama vimechomwa moto au vimeibiwa.
|
No comments:
Post a Comment