|
WAKAZI wa Kibamba, Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam, usiku wa
kuamkia jana walilazimika kuzikimbia nyumba zao baada ya kutokea
kishindo kikubwa cha milipuko katika kambi ya vifaru vya Jeshi la
Wananchi Tanzania (JWTZ) Mloganzila.
Tukio hilo limetokea majira ya usiku kati ya saa 5 hadi 7:04 ambapo
milipuko mitano ya mizinga ilisikika kutoka eneo hilo la Mlongazila
katika wilaya jirani ya Kisarawe mkoani Pwani, ikiambatana na kukatika
kwa umeme, mawasiliano ya simu na mvua kubwa.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na Tanzania Daima, wakazi hao
walisema tukio hilo limewashtua kwa sababu halijawahi kutokea katika
kipindi cha miaka zaidi ya saba walichoishi kwenye eneo hilo.
Walisema kuwa waliamua kukimbia na kuelekea kusikojulikana kwa lengo
la kuokoa maisha yao, kwani walihofia madhara ya milipuko ya mabomu
kama ilivyotokea kwenye kambi za Mbagala na Gongo la Mboto.
Mmoja wa wakazi hao, Mhando Yahaya, alisema wakazi wote wa Kibamba
walikimbilia kwenye kijiji kidogo cha Kibwegele, wakiacha nyumba pamoja
na mali zao bila kujali.
“Ujue serikali inabidi itowe angalizo kabla na si kufanya siri kwa
kuwa matokeo yake ni kama haya, wananchi tunatishika na kukimbia hovyo
usiku huu, mvua na giza vikituandama,” alisema Yahaya.
Naye Egnes Habiyu, alisema milipuko kama hiyo, imesababisha baadhi ya
wagonjwa wa moyo kushtuka hadi kufikia hatua ya kuishiwa nguvu na
wengine kujeruhiwa wakati wakikimbia.
Akifafanua kuhusu milipuko hiyo, Msemaji wa JWTZ, Kanali Kapambala
Mgawe, alisema hayo yalikuwa mazoezi ya kawaida na kwamba hayana
uhusiano wowote wa kivita.
Vilevile aliwatoa wasiwasi wananchi kuwa milipuko hiyo haina madhara bali ni moja ya mazoezi ya kawaida.
Kanali Mgawe alisema taarifa zilitolewa mapema kwa wakazi wanaoishi
jirani na kambi hiyo, hivyo kwa vile mazoezi yalifanyika usiku kukiwa
kumetulia sauti ya milipuko hiyo ilisikika hadi mbali.
|
No comments:
Post a Comment