Friday, August 3, 2012

CHADEMA waitaka CCM kuvunja Bunge


CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimekitaka Chama Cha Mapinduzi (CCM) na viongozi wake kulivunja Bunge ikiwa kina ujasiri, uzalendo na uadilifu ili kuwezesha mabadiliko ya mfumo wa utawala.
Kauli hiyo imetolewa na Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa CHADEMA, John Mnyika kwenye taarifa yake kwa vyombo vya habari akielezea kauli ya CCM iliyotolewa na Katibu wake wa Itikadi na Uenez Nape Nnauye na kusema inapaswa kuwa katika vitendo zaidi kwa kuwavua uanachama viongozi waliotuhumiwa kwa ufisadi tangu mwaka 2007.
“CHADEMA kinaukumbusha umma kauli ya Mwalimu Nyerere kwamba chama legelege, huzaa serikali legelege, matokeo ya hali hiyo ni kuwa Bunge legelege, hali hii inajidhihirisha kwa CCM kushindwa kushughulikia tuhuma za ufisadi dhidi ya viongozi wake ndani ya chama, Serikali na Bunge hali inayoathiri uwezo na uadilifu wa vyombo vya uchunguzi na kuchukua hatua zinazostahili,” alisema Mnyika.
Alisema CCM imeshindwa kusimamia misingi ya kupambana na rushwa kwa kutumia wingi wa wabunge wake kupitisha baadhi ya watuhumiwa wa ufisadi nchini kuwa viongozi wa kamati muhimu za Bunge na kuwataja baadhi yao kuwa ni Kamati ya Mambo ya nje, Ulinzi na Usalama ambayo mwenyekiti wake ni Edward Lowassa na Kamati ya Fedha na Uchumi, mwenyekiti wake ni Andrew Chenge.
Mnyika pia aliutaka umma upuuzie kauli ya CCM ya kulipongeza Bunge kwa kusimamia rasilimali za nchi na kuhakikisha nchi inapiga hatua kimaendeleo, badala yake CHADEMA itaanza kuunganisha nguvu ya umma kutaka kamati zote za Bunge zivunjwe na kuundwa upya ili kuurejesha mhimili huo kwenye mwelekeo unaostahili.

No comments:

Post a Comment