|
HATIMAYE mshambuliaji Mrisho Ngassa wa timu ya Azam FC,
amepelekwa Simba kwa kitita cha sh mil. 25, kiasi ambacho kimeafikiwa na
klabu yake iliyomsajili msimu wa 2009/10 kutoka Yanga kwa dau la sh
mil. 59.
Habari zilizoifikia Tanzania Daima jana jioni, zilisema kuwa suala
hilo limefanyika baada ya kikao cha pamoja kati ya Azam na Simba
kilichofanyika jana.
Simba imemtwaa nyota huyo siku moja tu tangu uongozi wa Azam umweke
sokoni kwa sh mil. 50, wakikerwa na mchezaji huyo kuonesha mapenzi yake
kwa timu yake ya zamani ya Yanga.
Habari za awali ambazo ziliifikia Tanzania Daima, zilisema licha ya
Azam kuweka dau hilo, hadi jana mchana timu za Simba na Yanga, zilikuwa
tayari kumsajili kwa dau tofauti.
Wakati Yanga wakitenga kiasi cha shilingi mil. 20 kumrejesha nyota
huyo kundini, Simba wao wapo tayari kutoa kiasi cha sh mil. 25 kwa ajili
ya kuichezea kwa miaka miwili.
Kabla ya kwenda mitamboni, Meneja wa Azam FC, Patrick Kahemele,
kupitia mtandao wa kijamii, alikiri klabu za Simba na Yanga kumtaka, pia
zikitofautiana kwa dau.
“Hadi hivi sasa ofa ya Simba ni sh mil. 25 na Yanga sh mil. 20.
Kutokana na hilo, Simba wapo kwenye nafasi kubwa ya kumnyakua Ngasa
(Mrisho). Kesho (leo) ni siku ya mwisho. Ingawa tungependa kumuuza
Yanga, lakini tutampeleka kwa timu yenye ofa nzuri zaidi,” alisema
Kahemele na kusisitiza.
“Lengo la Azam lilikuwa ni kumpeleka Mrisho kwenye timu ambayo
atacheza kwa raha na amani, kutokana na yeye kuivaa na kuibusu jezi ya
Yanga siku ambayo Azam FC haikuwa na mchezo na Yanga….. Azam FC
inaamini kuwa Yanga ilikuwa sehemu sahihi kwa Mrisho, lakini uongozi wa
Yanga umeonekana kutokuwa na haja naye, ndiyo maana umeonekana kukataa
kutoa ofa ya maana.
“Kutokana na sababu hizo, Azam FC italazimika kumuuza Simba, kwani
hatuhitaji kuwa na mchezaji ambaye anafanya vitendo vya kuidharau
‘brand’ ya Azam FC ambayo tunajaribu kuijenga,” alisema Kahemele.
Kitendo cha Azam kuamua kumuuza nyota huyo Simba kwa kigezo tu cha dau
kubwa bila kuzingatia mapenzi ya mchezaji, hakina tofauti ya mchezaji
huyo kuuzwa kama kifurushi ambacho mwelekeo wake hutegemea matakwa ya
mbebaji.
Juhudi za kumtafuta nyota huyo kupata msimamo wake juu ya maamuzi hayo
yaliyofanywa na Azam na Simba, jana ziligonga ukuta kwani simu yake
ilikuwa haipo hewani.
Katika hatua nyingine, baadhi ya wachezaji wa timu ya Azam wamesikitishwa na kitendo
cha klabu hiyo kumtimua Kocha Mkuu, Stewart Hall, wakisema ni kati ya makocha bora, hivyo uamuzi wa kumfukuza si sahihi.
Kauli ya wachezaji hao inatokana na kocha huyo kuipatia mafanikio
makubwa timu hiyo ikiwamo kuiwezesha kushika nafasi ya pili katika Ligi
Kuu ya Bara, pia nafasi ya pili kwenye michuano ya Kombe la Kagame nyuma
ya Yanga, licha ya kushiriki mara ya kwanza.
|
No comments:
Post a Comment