Friday, August 3, 2012

Mrisho Ngasa auzwa Simba kama kifurushi



HATIMAYE mshambuliaji Mrisho Ngassa wa timu ya Azam FC, amepelekwa Simba kwa kitita cha sh mil. 25, kiasi ambacho kimeafikiwa na klabu yake iliyomsajili msimu wa 2009/10 kutoka Yanga kwa dau la sh mil. 59.
Habari zilizoifikia Tanzania Daima jana jioni, zilisema kuwa suala hilo limefanyika baada ya kikao cha pamoja kati ya Azam na Simba kilichofanyika jana.
Simba imemtwaa nyota huyo siku moja tu tangu uongozi wa Azam umweke sokoni kwa sh mil. 50, wakikerwa na mchezaji huyo kuonesha mapenzi yake kwa timu yake ya zamani ya Yanga.
Habari za awali ambazo ziliifikia Tanzania Daima, zilisema licha ya Azam kuweka dau hilo, hadi jana mchana timu za Simba na Yanga, zilikuwa tayari kumsajili kwa dau tofauti.
Wakati Yanga wakitenga kiasi cha shilingi mil. 20 kumrejesha nyota huyo kundini, Simba wao wapo tayari kutoa kiasi cha sh mil. 25 kwa ajili ya kuichezea kwa miaka miwili.
Kabla ya kwenda mitamboni, Meneja wa Azam FC, Patrick Kahemele, kupitia mtandao wa kijamii, alikiri klabu za Simba na Yanga kumtaka, pia zikitofautiana kwa dau.
“Hadi hivi sasa ofa ya Simba ni sh mil. 25 na Yanga sh mil. 20. Kutokana na hilo, Simba wapo kwenye nafasi kubwa ya kumnyakua Ngasa (Mrisho). Kesho (leo) ni siku ya mwisho. Ingawa tungependa kumuuza Yanga, lakini tutampeleka kwa timu yenye ofa nzuri zaidi,” alisema Kahemele na kusisitiza.
“Lengo la Azam lilikuwa ni kumpeleka Mrisho kwenye timu ambayo atacheza kwa raha na amani, kutokana na yeye kuivaa na kuibusu jezi ya Yanga siku ambayo Azam FC haikuwa na mchezo na Yanga….. Azam FC inaamini kuwa Yanga ilikuwa sehemu sahihi kwa Mrisho, lakini uongozi wa Yanga umeonekana kutokuwa na haja naye, ndiyo maana umeonekana kukataa kutoa ofa ya maana.
“Kutokana na sababu hizo, Azam FC italazimika kumuuza Simba, kwani hatuhitaji kuwa na mchezaji ambaye anafanya vitendo vya kuidharau ‘brand’ ya Azam FC ambayo tunajaribu kuijenga,” alisema Kahemele.
Kitendo cha Azam kuamua kumuuza nyota huyo Simba kwa kigezo tu cha dau kubwa bila kuzingatia mapenzi ya mchezaji, hakina tofauti ya mchezaji huyo kuuzwa kama kifurushi ambacho mwelekeo wake hutegemea matakwa ya mbebaji.
Juhudi za kumtafuta nyota huyo kupata msimamo wake juu ya maamuzi hayo yaliyofanywa na Azam na Simba, jana ziligonga ukuta kwani simu yake ilikuwa haipo hewani.
Katika hatua nyingine, baadhi ya wachezaji wa timu ya Azam wamesikitishwa na kitendo cha klabu hiyo kumtimua Kocha Mkuu, Stewart Hall, wakisema ni kati ya makocha bora, hivyo uamuzi wa kumfukuza si sahihi.
Kauli ya wachezaji hao inatokana na kocha huyo kuipatia mafanikio makubwa timu hiyo ikiwamo kuiwezesha kushika nafasi ya pili katika Ligi Kuu ya Bara, pia nafasi ya pili kwenye michuano ya Kombe la Kagame nyuma ya Yanga, licha ya kushiriki mara ya kwanza.

No comments:

Post a Comment