|
ZAIDI ya robo tatu ya wagombea wa nafasi mbalimbali ndani ya
Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) Iringa, wamedaiwa
kudanganya umri wao wakati wa ujazaji wa fomu za kuwania nafasi hizo.
Kashfa hiyo imeibuka baada zoezi la uchukuaji na urejeshaji wa fomu kumalizika juzi.
Uchunguzi uliofanywa na Tanzania Daima Jumatano, umebaini kuwepo kwa
udanganyifu wa umri ambao kikomo chake ni miaka (30), huku baadhi ya
wagombea wakiwa na umri mkubwa zaidi ya hapo.
Udanganyifu huo wa UVCCM, umesababishwa na ushindani mkubwa uliopo
katika jumuiya nyingine za chama hicho mkoani hapa huku nafasi nyeti
zote za jumuiya hizo kama ile ya Jumuia ya Wazazi (TAPA) na Umoja wa
Wanawake Tanzania (UWT), zikienda kwa vigogo.
Mmoja kati ya vijana wanaowania nafasi moja wapo ndani ya UVCCM mkoani
hapa ambaye hakupenda kutaja jina lake kwenye vyombo vya habari,
alisema UVCCM Iringa imeendelea kupoteza dira yake huku kanuni za umoja
huo zikiendelea kufinyangwa na waliopata kuwa viongozi wa umoja huo.
Alisema, viongozi hao bado wanaonekana kung’ang’ania uongozi katika
kundi hilo la vijana japo umri wao umevuka hata kwa mwonekano wa kawaida
bila uthibitisho wa vyeti vya kuzaliwa.
Mgombea huyo alisema inashangaza kuona vijana wengi wakitumia vyeti
vya kuapa mahakamani badala ya vile walivyotumia kipindi cha nyuma
ambacho walipata kuomba nafasi za uongozi ndani ya UVCCM na jumuiya
nyingine za chama.
“Hivi tunaomba uongozi wa UVCCM mkoa kuwahoji wanachama waliokimbilia
kuziba nafasi za vijana wenye sifa ndani ya UVCCM kwa kudanganya miaka
yao ya kuzaliwa ...kwani haiwezekani kijana aliyegombea nafasi ya
uongozi ndani ya UVCCM mwaka 2007 akiwa na miaka 28 au 27, leo anakuja
kugombea tena akiwa na miaka pungufu ya hiyo.
“Ina maana alisimama kukua ili kuja kugombea nafasi hiyo?” alihoji
kijana huyo huku akiutupia lawama uongozi wa UVCCM mkoa kukubali kupokea
fedha za gharama za fomu kwa wanachama wa UVCCM ambao umri wao umevuka
mipaka.
Alisema wapo baadhi ya wagombea waliogombea nafasi za uenyekiti mwaka
2007 wakiwa wamejaza miaka 29, lakini leo wamekuja na umri mdogo zaidi.
Katibu wa UVCCM Iringa, Rhoda George, alisema kila mwanachama wa UVCCM mwenye sifa ya kugombea, anaruhusiwa kuchukua fomu.
Alisema hadi mwanachama kupitishwa kuwa kiongozi, vipo vikao
mbalimbali vya uchujaji wa majina ya wagombea ambavyo vinapitia sifa za
wote walioomba na iwapo itabainika wamedanganya basi vikao vitaamua.
|
No comments:
Post a Comment