Wednesday, December 5, 2012

Mnyika apeleka hoja ya maji Halmashauri


MBUNGE wa Jimbo la Ubungo (CHADEMA), John Mnyika, jana aliwasilisha katika Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam hoja binafsi inayohusu uboreshaji wa huduma ya majisafi na uondoaji wa majitaka katika maeneo mbalimbali jijini.
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, iliyotumwa na Katibu wa Mbunge Aziz Himbuka, alisema lengo la hoja hiyo ni kupendekeza baraza la madiwani wa jiji, kujadili na kupitisha maazimio ya hatua za haraka zaidi za kuboresha upatikanaji wa maji safi na ushughulikiaji wa maji taka katika Jimbo la Ubungo na jiji katika masuala yaliyo chini ya mamlaka ya halmashauri.
Mnyika alisema ameamua kuchukua hatua hiyo wakati huu ili Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam iweze kutimiza wajibu wake mwezi huu, huku akisubiri kuwasilisha hoja binafsi bungeni katika mkutano wa kumi Februari 2013 endapo Wizara ya Maji haitachukua hatua zinazostahili.
Alisema pamoja na mafanikio ya kawaida yaliyopatikana kupitia mikutano yake na wananchi katika kata mbalimbali jimboni kwake, ufuatiliaji serikalini bado una matatizo yanayohitaji baraza la madiwani kushughulikia kwa ajili ya Jimbo la Ubungo na Mkoa mzima wa Dar es Salaam.
Mbunge huyo alisema kufuatilia masuala ya maji, alianza kwa kufanya kongamano la Maji katika Jimbo la Ubungo mwanzoni mwa mwaka 2011 ili kuwakutanisha wananchi, mamlaka husika na wadau wengine katika kuunganisha nguvu kupata ufumbuzi.
Alizitaja hatua nyingine ambazo amekwishazichukua ili ziweze kufanyiwa haraka ni pamoja na kuishirikisha DAWASA, DAWASCO na Wizara ya Maji ambao alidai utekelezaji wao ulikuwa mdogo na kwamba mpaka sasa hakuna ambacho kimeishafanyika.
Hivyo, Mnyika alisema kutokana na hilo aliamua kukusanya nguvu ya pamoja kufanya maandamano ya kudai maji hadi katika ofisi kuu za DAWASCO.
“Maandamano hayo yalizaa matunda kwa upande wa DAWASCO ambapo ameshafanya nao ziara ya kikazi ya kata mbalimbali ya kutembelea maeneo yenye matatizo na hatua zimechukuliwa ambazo zimewezesha baadhi ya maeneo kuanza kutoka maji,” ilisema taarifa yake.
Hata hivyo alisema bado yapo maeneo mengi yenye matatizo makubwa ya maji ikiwemo ya Msumi, Makabe, Msakuzi, Malambamawili, Msingwa, Goba na mengineyo mengi katika jiji la Dar es salaam.

No comments:

Post a Comment