Wednesday, December 5, 2012

Dk. Slaa, Nape jino kwa jino






KATIBU wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, amesema anampongeza Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Wilbrod Slaa, kwa kukiri kwamba anamiliki kadi ya CCM hadi leo.
“Kwanza nampongeza kwa kuanza kujifunza kusema ukweli maishani mwake, bila shaka ametambua kuwa uongo haulipi. Kitendo cha kukiri anamiliki kadi ya CCM bado ni cha kiungwana, nampongeza kwa hili,” alisema Nape, baada ya mwandishi wetu kumtaka maoni yake juu ya Dk. Slaa kukiri kumiliki kadi ya CCM hadi sasa.
Akijibu tuhuma za Nape alizotoa juzi kwamba baadhi ya vigogo wa CHADEMA akiwemo Dk. Slaa, bado wana kadi za CCM na baadhi yao wanaendelea kuzilipia, Katibu huyo wa CHADEMA kupitia vyombo vya habari, amekiri kuwa anayo kadi ya CCM na kwamba anaitunza kama kumbukumbu muhimu kwake.
Pia Dk. Slaa alisema Nape anapiga mayowe na kumtaka asiwapotezee muda Watanzania kwa kujadili mambo yasiyo na msingi na kuacha kujadili suala la umaskini na jinsi ya kuwasaidia kuondokana na hali hiyo.
Pamoja na pongezi hizo, Nape amemtaka Dk. Slaa kuwaambia Watanzania kwamba kadi hiyo ameilipia mpaka lini, pia aache tabia ya kuwadanganya wenzake kurudisha kadi zao za CCM huku yeye akibaki na yake kibindoni.
“Ni vizuri sasa Dk. Slaa awaambie Watanzania amelipia mpaka lini kadi hii. Lakini aache kuwadanganya wenzake kurudisha kadi zao huku yeye akibaki na yake huu ni unafiki,” alisema Nape.
Aidha Nape ambaye amekiri kumheshimu sana Dk. Slaa kama Babu yake, amesema alishtuka sana kusikia Katibu Mkuu huyo wa CHADEMA akiwatuhumu viongozi wa chama hicho, hivi karibuni kuwa ni mamluki wa CCM huku akijua yeye ni mamluki namba moja kwani wenzie hawana kadi za CCM yeye anayo.
“Nimesikia anahoji hili linawasaidiaje Watanzania maskini! Swali hili limethibitisha upeo mdogo sana wa kufikiri wa kiongozi mkubwa na ninayemheshimu kama huyu. Lazima ajue kwamba yeye anaomba kuwa kiongozi, hivyo lazima wananchi tumjue tabia zake,” alisema Nape na kuongeza:
“Viongozi wanafiki wa aina yake ni janga kwa taifa letu.Usipokuwa mwaminifu kwa kidogo huwezi kuwa mwaminifu kwa kikubwa. Lazima anayetaka kuwa kiongozi aishi anayoyasema.”

No comments:

Post a Comment