|
KATIBU wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM wa Itikadi na Uenezi,
Nape Nnauye, amesema anampongeza Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Wilbrod
Slaa, kwa kukiri kwamba anamiliki kadi ya CCM hadi leo.
“Kwanza nampongeza kwa kuanza kujifunza kusema ukweli maishani mwake,
bila shaka ametambua kuwa uongo haulipi. Kitendo cha kukiri anamiliki
kadi ya CCM bado ni cha kiungwana, nampongeza kwa hili,” alisema Nape,
baada ya mwandishi wetu kumtaka maoni yake juu ya Dk. Slaa kukiri
kumiliki kadi ya
CCM hadi sasa.
Akijibu tuhuma za Nape alizotoa juzi kwamba baadhi ya vigogo wa
CHADEMA akiwemo Dk. Slaa, bado wana kadi za CCM na baadhi yao
wanaendelea kuzilipia, Katibu huyo wa CHADEMA kupitia vyombo vya habari,
amekiri kuwa anayo kadi ya CCM na kwamba anaitunza kama kumbukumbu
muhimu kwake.
Pia Dk. Slaa alisema Nape anapiga mayowe na kumtaka asiwapotezee muda
Watanzania kwa kujadili mambo yasiyo na msingi na kuacha kujadili suala
la umaskini na jinsi ya kuwasaidia kuondokana na hali hiyo.
Pamoja na pongezi hizo, Nape amemtaka Dk. Slaa kuwaambia Watanzania
kwamba kadi hiyo ameilipia mpaka lini, pia aache tabia ya kuwadanganya
wenzake kurudisha kadi zao za CCM huku yeye akibaki na yake kibindoni.
“Ni vizuri sasa Dk. Slaa awaambie Watanzania amelipia mpaka lini kadi
hii. Lakini aache kuwadanganya wenzake kurudisha kadi zao huku yeye
akibaki na yake huu ni unafiki,” alisema Nape.
Aidha Nape ambaye amekiri kumheshimu sana Dk. Slaa kama Babu yake,
amesema alishtuka sana kusikia Katibu Mkuu huyo wa CHADEMA akiwatuhumu
viongozi wa chama hicho, hivi karibuni kuwa ni mamluki wa CCM huku
akijua yeye ni mamluki namba moja kwani wenzie hawana kadi za CCM yeye
anayo.
“Nimesikia anahoji hili linawasaidiaje Watanzania maskini! Swali hili
limethibitisha upeo mdogo sana wa kufikiri wa kiongozi mkubwa na
ninayemheshimu kama huyu. Lazima ajue kwamba yeye anaomba kuwa kiongozi,
hivyo lazima wananchi tumjue tabia zake,” alisema Nape na kuongeza:
“Viongozi wanafiki wa aina yake ni janga kwa taifa letu.Usipokuwa
mwaminifu kwa kidogo huwezi kuwa mwaminifu kwa kikubwa. Lazima anayetaka
kuwa kiongozi aishi anayoyasema.”
|
No comments:
Post a Comment