Wednesday, December 5, 2012

CCM haiwezi kupambana na rushwa – Msigwa






MBUNGE wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa (CHADEMA), amesema Chama cha Mapinduzi (CCM) hakitaweza kufanikiwa kupambana na kuzuia rushwa nchini, kutokana na viongozi wengi wa chama hicho kupatikana kwa njia ya rushwa.
Msigwa aliyasema hayo wakati wa mkutano wa hadhara uliofanyika juzi katika viwanja vya Mwembetogwa mkoani hapa.
Mbali na Msigwa kuinyooshea kidole CCM kwa rushwa, Mkurugenzi wa Kampeni na Uchaguzi CHADEMA, Msafiri Mtemelwa, alisema wakati wa Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, chama hicho tawala hakikuwa kama kilivyo sasa.
Alisema CCM ilikuwa ina maadili mema, lakini hivi sasa kila kona nchini imejaa rushwa ambayo inasababisha adha kubwa kwa maskini.
Aliongeza kuwa licha ya michakato mbalimbali ya kukibadili chama kwa maana ya viongozi kama njia ya kukisafisha, wamekuwa wakisahau kuwa wanaowapatia uongozi ni watu ambao tayari walishaiingiza nchi pabaya.
“Leo mmeambiwa viongozi wa CCM wamewabadilisha! Wamewabadilishieni kanzu lakini mapadre au mashehe ni wale wale, Kinana ambaye aliaga siasa basi anastaafu, leo amerudi kufuata nini?” alisema Mtemelwa.
Akitolea mfano kwa baadhi ya viongozi ambao wameipeleka nchi pabaya, alimtaja aliyekuwa Katibu Mkuu wa CCM, Philip Mangula, akiwa na mwenyekiti wake Benjamin Mkapa akidai kuwa walichangia kwa kiasi kikubwa kuiyumbisha nchi.
“Mkapa na Mangula ndio walioifilisi nchi hii. Mangula aliuza nyumba za serikali akiwa Katibu Mkuu na Mwenyekiti akiwa Mkapa. Mangula pia aliuza machimbo ya almasi katika nchi hii yeye akiwa Katibu Mkuu na Mwenyekiti akiwa Mkapa,” alisema.
Hata hivyo alidai kuwa Mwalimu Nyerere aliacha machimbo ya madini maeneo mawili, Buhemba na Shinyanga Mwadui, lakini Rais Jakaya Kikwete na wenzake wameuza North Mara Lyamungo pamoja na Buhemba mkoani Mara huku wananchi wakiendelea kulia njaa.
Alieleza kuwa taifa la Tanzania ni taifa tajiri duniani kuliko sehemu nyingine yoyote isipokuwa linakosa viongozi wenye maadili bora wa kusimamia rasilimali hizo kwa manufaa ya taifa.
Aidha amewataka Watanzania hususan vijana kuchukua hatua za haraka za kuchagua viongozi makini ili kuinusuru nchi kutoka mikononi mwa viongozi wanaofanya kazi kwa maslahi binafsi na kuhakikisha Kikwete ndiye Rais wa mwisho nchini kutoka CCM.

No comments:

Post a Comment